Mbunge wa CHADEMA anusurika kukatwa mapanga
Polisi wakwepa kukamata diwani wa CCM
MBUNGE wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, amenusurika
kucharangwa mapanga, baada ya kundi la vijana wanaoaminika kuwa wafuasi
wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kumvamia baada ya kukerwa na hatua ya
kuhama kwa karibu uongozi mzima wa chama hicho Kata ya Nduli.
Kundi hilo lilimvamia Msigwa alipokuwa akijiandaa kuondoka akiwa na
viongozi wanane waliokuwa wa CCM wa kata hiyo, ambao walihamia CHADEMA
jana, ambapo walianza kuwashambulia watu walioandamana naye na
kuwajeruhi vibaya kwa mapanga watu wawili, kiasi cha kulazimika
kukimbizwa hospitalini kwa matibabu.
Polisi ambao walipigiwa simu mara baada kuanza kwa vurugu hizo,
hawakuweza kujitokeza, hali iliyozusha taharuki kubwa kutoka kwa
wananchi waliolazimika kukimbia ovyo ili kuokoa maisha yao. Vijana
wanaodaiwa kuumizwa vibaya zaidi ni Oscar Sanga na Seleman Komba, ambao
walikuwa miongoni mwa wananchi waliohudhuria mkutano huo.
Taarifa za awali zimedai kuwa kundi hilo la vijana lilitumwa na mmoja
wa viongozi wa ngazi ya juu wa chama hicho, kwa madai ya kukasirishwa na
hatua ya kuhama kwa mwenyekiti, katibu na wajumbe sita wa CCM Kata ya
Nduli, ambao waliwaongoza zaidi ya wanachama 90 kukihama chama hicho na
kujiunga na CHADEMA.
Mchungaji Msigwa ambaye aliandamana na Diwani wa Kata ya Mivinjeni,
Frank Nyalusi (CHADEMA), alifanya mkutano huo akilenga kuwataka wananchi
wawe jasiri wa kutambua haki zao na kudai maelezo sahihi ya matumizi
ya fedha za miradi ya maendeleo inayotolewa na serikali katika ngazi za
kata na vijiji.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa, Evarist Mangalla, hakuweza
kupatikana mara moja kuzungumzia vurugu hizo, lakini mmoja wa maofisa wa
jeshi hilo alidai hawana taarifa na kwamba watazifuatilia kwa makini
kujua kilichotokea na kuahidi kuchukua hatua za kisheria kwa waliohusika
na vurugu hizo.
Wakizungumza mara baada ya kujiunga na CHADEMA, aliyekuwa mwenyekiti
wa CCM wa kata hiyo, Ayub Mwenda na katibu wake, Godwin Sanga, walisema
kuwa wao na viongozi wameamua kukihama chama hicho, baada ya kugundua
kuwa kimejaa viongozi wasiokuwa wakweli na wasiojali maendeleo ya
wananchi waliowapigia kura.
Mwenda pamoja na aliyekuwa mjumbe wa kata hiyo, Temina Ndete, walidai
kuwa kwa muda mrefu wamejitahidi sana kupigania haki za wanyonge, lakini
hawakuweza kufua dafu kwa sababu uongozi wa juu wa CCM umewatupa na
kujali masilahi ya wachache.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment