Nnauye: Mbowe wataje watakaohamia chadema

CHAMA Cha Mapinduzi(CCM) kimemtaka Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe kuwataja hadharani wabunge 70 kutoka na mawaziri saba wa CCM, ambao wameomba kujiunga na chama hicho cha upinzani ili kuuthibitishia umma kama alichochokisema kina ukweli.

Juzi, akihutubia mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya NMC, Unga Ltd jijini Arusha, Mbowe alisema idadi hiyo ya wabunge na mawaziri wanatarajia kujiunga Chadema siku za usoni na kutangaza chama hicho tayari kimevuna wanachama 10,400 kwa mkoa wa Arusha na Manyara.

Wanachama hao ni kutoka Ngorongoro (2,500), Monduli (2,000), Longido (800), Arumeru (1,200) Arusha mjini (2,600) na Simanjiro (1,300).

Jana, akizungumza na Mwananchi, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema kama Mbowe ana uhakika na anachokisema ni bora angesubiri kitokee halafu ndiyo azungumze vinginevyo awataje wanachama hao ili umma umuamini."Anachokizungumza hakina msingi na hoja zake hazina mashiko.

Anachokizungumza angekaa nacho kwanza ili kitokee na hivi sasa wananchi wa Arusha wana matatizo hawahitaji kujua na nani anatoka wapi na kwenda wapi," alisema Nape.Alisema chama makini hakiwezi kujitangaza kuwa kinachukua wanachama wa chama kingine, bali ni kutafuta wanachama wapya kwani Tanzania ina watu zaidi ya milioni 40.

"Ninamshauri Mbowe aache kukurupuka na aache uongo, awataje hao anaowazungumzia na akiendelea na tabia ya aina hii itamshushia heshima,"alisema Nape na kuongeza;"Siasa za aina hii amuachie Dk Slaa kwani Mbowe yeye ni mwenyekiti wa chama na kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni anaheshimika.


"Nape alisema ni muhimu Mbowe akaacha kukurupuka kwa kutoa hoja bila mpangilio kwani heshima aliyonayo itashuka akiendelea na hali hiyo.Juzi mbowe alitumia mkutano huo kuwatoa hofu wana Chadema wanaotilia shaka wimbi la viongozi na wana CCM wanaojiengua na kujiunga na chama hicho kikuucha upinzani kuwa Chadema iko imara na hakiwezi kuhujumiwa wala kupenyezewa mamluki kama baadhi wanavyodhani.

Mbowe alitamba kuwa ameongoza harakati za upinzani kwa zaidi ya miaka 20 sasa, ambayo imeanza kuzaa matunda kwa Watanzania kukiamini Chadema hivyo hawezi kukubali kuruhusu mtu yeyote yule anayetumia njia ya wazi au ya kificho kukidhoofisha.

Nassari, Heche matataniKatika hatua nyingine, jeshi la polisi mkoani Arusha linawasaka kwa mahojiano mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari na Mwenyekiti wa Taifa wa Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha), JohnHeche kuhusiana na kauli walizotoa kwenye mkutano huo wa hadhara uliofanyika juzi kwenye uwanja wa Unga LtD.

Habari zilizopatikana kutoka ndani ya jeshi la polisi na baadaye kuthibitishwa na Kaimu Kamanda wa polisi mkoa wa Arusha, Akili Mpwapwa zimeeleza kuwa kwenye orodha hiyo ya viongozi wanaosakwa pia yumo aliyekuwa mjumbe wa mkutano mkuu wa taifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ally Bananga aliyehamia Chadema hivi karibuni.

Akizungumza kwa njia ya simu jana, Kamanda Mpwapwa alisema viongozi hao walitoa maneno yanayoelekea kuwa ya uchochezi ambayo hayawezi kuachwa bila wahusika kuhojiwa kujua walichomaanisha.

“Kwani wewe hukuwepo pale uwanja jana (juzi) wakati viongozi wa Chadema walipokuwa wakihutubia? Walitoa maneno ambayo lazima tuwahoji kujiridhisha walichomaanisha na hili ni jukumu la kawaida la kiuchunguzi la polisi,” alisema Kamanda MpwapwaKaimu Kamanda huyo ambaye amaeteuliwa kuwa Kamanda wa polisi mkoa wa Manyara katika uteuzi na mabadiliko yaliyofanywa juzi na Inspekta Jenerali wa polisi nchini (IGP), Said Mwema alisema hatua zaidi dhidi ya viongozi na mwanachama huyo mpya wa Chadema itajulikana baada ya kuhojiwa.

“Siwezi kukanusha wala kuthibitisha iwapo tutawafungulia mashtaka kwa kauli hizo tunazozichunguza, uamuzi utategemeana na maelezo yao na taarifa za uchunguzi tunazoendelea kukusanya,” alisema Mpwapwa.

Katika mkutano huo wa hadhara, viongozi kadhaa wa Chadema walioongozwa na Mbowe walihutubia na kutoa kauli mbalimbali huku Nassari akitumia fursa hiyo kuzungumzia utendaji wake ndani ya bunge mara alipoapishwa baada ya kuibuka mshindi katika uchaguzi mdogo uliofanyika Aprili Mosi, mwaka huu.

Mbunge huyo kijana aliueleza umati mkubwa uliohudhuria mkutano huo uliolenga kuzindua oparesheni ‘Vua gamba, vaa gwanda’ kuwa jeshi la polisi linapaswa kuongeza juhudi katika upelelezi na uchunguzi wa mauaji wa aliyekuwa mwenyekiti wa Chadema, Kata ya USA-River, Msafiri Mbwambo aliyechinjwa kwa nyuma na kitu chenye ncha kali.

Nassari alisema uvumilivu wa wana Chadema kuendelea kusubiri kwa muda mrefu uchunguzi wa mauaji hayo ya kinyama unakaribia kufikia kikomo kwa sababu wauaji walitumia simu kumwita marehemu hivyo, ni rahisi kwa vyombo vya dola kufuatilia namba hiyo na kutambua wahusika kirahisi.

Pengine kauli inayowezekana kumponza hadi kuitwa kwa mahojiano polisi ni madai yake kuwa iwapo vyombo vya dola na serikali vitaendeleza ukandamizaji dhidi ya wanaopigania haki, usawa na ustawi wa jamii kama inavyoshuhudiwa sehemu mbalimbali nchini, basi watatangaza Arusha kuwa eneo linalojitegemea yeye akiwa Rais na aliyekuwa mbunge wa Arusha mjini, Godbless Lema akiwa Waziri Mkuu.

Hata hivyo, Mbowe alifuta kauli hiyo aliposimama kuhutubia akisema Chadema inahitaji kuunganisha na kukomboa nchi yote bila kuacha kipande chochote akisema kauli ya Nassari ilitokana na hamasa ya kisiasa jukwaani.

Kwa upande wake, Bananga yeye alitumia fursa hiyo kuwaomba radhi wana Chadema wote aliowakwaza kwa vitendo vyake alipokuwa CCM na papo hapo akamshukuru Rais Jakaya Kikwete na mtoto wake, Ridhwani kwa kile alichodai kukamsirisha na kumpa mwanya wa kufikiri sawa sawa na kujiunga Chadema alichogundua ndicho chama chenye dhamira ya kweli ya kukomboa taifa.

Heche yeye aliueleza umati huo kuwa ataanza oparesheni hiyo katika mikoa ya Kusini kwa lengo la kukisambaratisha CCM na kukiimarisha Chadema huku akisema, Rais Kikwete ameonyesha dharau kubwa kwa umma unaolalamikia maisha magumu na kupanda kwa gharama za maisha kwa kuzidisha ukubwa wa baraza la mawaziri kwa kuteua mawaziri watano zaidi ya waliokuwepo awali.

Katika hatua nyingine, maelfu ya wakazi wa Karatu, jana walijitokeza kumpokea Mbunge mteule wa viti maalum wa Wilaya ya Karatu, Cecilia Pareso.Pia katika mkutano huo, Chadema walitoa tamko la kuitaka Serikali kuwafikisha mahakamani mawaziri wote waliondolewa kutokana na ubadhirifu la sivyo chama hicho, kitaandaa maandamano yasiyo na ukomo nchi nzima.

Mjumbe wa Kamati Kuu Godbless Lema alisema haiwezekani mawaziri wabainike wamesababisha upotevu wa fedha za zaidi ya Sh9 trilioni, wakaondolewa uwaziri tu huku mamia ya watu ambao wametuhumiwa kwa wizi wa simu wanaozea magereza. “Tunasema hivi, hawa mawaziri wote waliobainika kusababisha hasara kwa taifa lazima wafikishwe kwenye vyombo vya sheria na kuvuliwa ubunge,” alisema Lema.

Alisema Sh9 trilioni zinatosha kutengeneza barabara za lami katika mikoa yote nchini, au kujenga nyumba za walimu wote wa shule za sekondari na msingi.

No comments:

Post a Comment