Mbowe ambana Pinda polisi kuua raia

Kambi ya Upinzani bungeni imeitaka serikali kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa ahadi ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuchunguza vifo vya raia vilivyotokea mikononi mwa askari polisi au vyombo vya dola. Julai mwaka jana, Pinda aliahidi kwamba serikali ingechunguza vifo hivyo kwa kutumia sheria ya Inquest kuchunguza mauaji ya raia wakiwa mikononi mwa vyombo vya dola.

Kiongozi wa Kambi ya Upinzani bungeni, Freeman Mbowe, akitoa maoni ya upinzani kuhusu makadirio ya Ofisi Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha wa 2012/13 alisema pamoja na ahadi hiyo, bado kumekuwepo na mauaji ya kutisha na ya kikatili kwa raia wakiwa mikononi mwa polisi. Alisema taarifa ya Haki za Binadamu na Utawala Bora zinaonyesha kwamba vifo hivyo vimekuwa vikiongezeka kila mwaka na hakuna hatua zozote zinazochukuliwa.

‘Ni muhimu tukatambua kuwa kila kifo cha mtu ni tofauti na cha mwingine, na hutokea katika mazingira tofauti. Hivyo, kwa kuzingatia kilio cha wananchi ambao Serikali ina wajibu wa kuwalinda, vifo vyote ambavyo vimetokea kwa sababu ya matumizi ya nguvu, kikiwamo kifo cha raia kilichotokea akiwa chini ya uangalizi wa vyombo vya dola, ni vema serikali ikazingatia mazingira husika,” alisema.

Alisema taarifa ya haki za binadamu ya mwaka jana inaeleza kwamba kuanzia Januari hadi Desemba 2011, takribani watu 25 wamefariki wakiwa mikononi mwa polisi na maafisa wengine wa ulinzi na matukio mengine yakiwaacha zaidi ya watu 50 na majeraha.

Alikumbusha kwamba ripoti hizo zinaonyesha mauaji ya raia mikononi mwa polisi yameendelea kuongezeka ambapo watu watano walifia mikononi mwa polisi mwaka 2008, watu 15 mwaka 2009 hadi watu 52 mwaka 2010 na katika kipindi cha Januari hadi Mei mwaka jana, watu 9 walikuwa wameripotiwa kuuawa katika eneo la Nyamongo, Tarime mkoani Mara.

“Kambi ya Upinzani tunatambua kuwa taarifa hizi za mauaji zinawagusa askari Polisi pia kwa kuwa kwa mwaka uliopita katika maeneo ya Tarime, Tabora, Shinyanga, Arusha na Rukwa polisi watano waliuawa na wananchi…tunaamini kuwa kuacha kuchukua hatua dhidi ya polisi wachache wanaolichafua jeshi la polisi kwa ujumla inasababisha picha mbaya ya taifa letu kitaifa na kimataifa,” alisema Mbowe.

Mbowe ambaye ni mbunge wa Hai (Chadema), alizungumzia pia unyanyasaji wa kisiasa unaowakuta wafuasi na viongozi wa vyama vya upinzani akieleza kwamba matukio hayo yamekuwa yakidhihirika zaidi kwenye chaguzi ndogo za madiwani, ubunge au vijiji na vitongoji hapa.

Alitolea mfano kujeruhiwa kwa wabunge wa Chadema wakati wa uchaguzi mdogo wa madiwani jijini Mwanza, Aprili mwaka huu (Highness Kiwia- Ilemelela na Salvatory Machemli- Ukerewe) walikatwa mapanga wakati wa uchaguzi mdogo wa Udiwani wa Kata ya Kirumba na wanaosadikiwa kuwa wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM). Alisema polisi wakishindwa kuzuia tukio hilo pamoja na kuwa walifika katika eneo la tukio tena wakiwa na silaha.

“Manyanyaso haya hayawezi kuvumiliwa tena ni lazima kama taifa tujue kuwa nchi hii ni ya vyama vingi vya siasa na hivyo kila raia ana haki ya kujiunga na chama chochote cha siasa bila shinikizo. Hii ni kwa sababu bado mikutano ya kisiasa na hata mikutano ya waheshimiwa wabunge wa upinzani inavamiwa mara kwa mara mathalani uvamizi aliofanyiwa Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa,” alisema Mbowe.

SHEREHE ZA UHURU, TAIFA
Akizungumzia maadhimisho mbalimbali, alisema siyo lazima sherehe zote zifanyike kila mwaka kwa kuwa zinatumia fedha nyingi bila tija huku akiitaka Serikali iweke wazi kiasi cha fedha kilichotumika kwenye maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 tangu Tanganyika ipate uhuru. Alisema gazeti moja liliripoti kwamba katika maadhimisho hayo, serikali ilitumia Sh. bilioni 64; taarifa ambazo hazikuwahi kukanushwa na serikali.

“Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali itoe tamko kuhusu matumizi hayo pamoja na mchanganuo wake ili kutekeleza dhana nzima ya uwazi na ukweli…taarifa za gharama za sherehe hizi za Kitaifa zikawekwa hadharani, zikiwemo gharama za mbio za mwenge ili umma wa Watanzania waweze kuchambua na kuona kama kweli bado ni tija na kipaumbele kwa Taifa kuendeleza sherehe hizi kwa mfumo tulio nao leo,” alisema.

Alizungumzia tatizo la chaguzi nchini na kusema kuwa kumekuwa na ushahidi kuwa watendaji wa serikali wamekuwa wakiingilia mchakato huo kwa faida ya chama tawala.

Alinukuu barua ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara, B.B Kichinda, ya Mei 23, mwaka huu yenye Kumb. Na FA.291/300/08/25 kwenda kwa Wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya na nakala zake kusambazwa kwa wakuu wote wa Wilaya za Mkoa wa Mara, iliyoeleza "Yah: Kusimamisha uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji katika mamlaka za serikali za mitaa"

Alisema katika barua hiyo, Kichinda aliwaelekeza watendaji hao kwamba chaguzi hizo zinasimamishwa ili kupisha uchaguzi wa CCM.

"Kwa barua hii ni dhahiri kuwa Katibu huyu amepewa maagizo kutoka ngazi ya juu na kwa mujibu wa tangazo la Serikali Na 51 la tarehe 17 Disemba, 2010 mwenye dhamana ya kutoa maelekezo hayo ni Waziri Mkuu kwani ndio msimamizi mkuu wa Tamisemi... barua hii ilifuatiwa na agizo la wakurugenzi watendaji wa Halmashauri mbalimbali za Wilaya za Mkoa wa Mara na kusimamisha chaguzi hizo," alisema.

Alimtaka Waziri Mkuu kutoa kauli ya Serikali juu ya kusimamishwa kwa chaguzi hizo ili kupisha uchaguzi wa CCM.